UPENDO WA MUNGU UANGAZE JUU YAKO

David Wilkerson (1931-2011)

Maneno haya ya Yesu yanagusa nafsi yangu: “Kwa hiyo msiwe na wasiwasi, mkisema, ‘Tutakula nini?’ au ‘Tunywe nini?’ au ‘Tuvae nini?’ Kwa maana watu wa mataifa mengine hutafuta mambo hayo yote. Kwa maana Baba yenu wa mbinguni anajua ya kuwa mnahitaji hayo yote” (Mathayo 6:31-32).

Yesu anaonya juu ya mwelekeo wa kipagani kuwa na wasiwasi. Anatuambia kwamba wasiwasi juu ya kazi yetu, familia, siku zijazo au kuishi ni njia ya maisha ya kipagani. Ni mtazamo wa wale ambao hawana Baba wa mbinguni. Hawamjui Mungu jinsi anavyotamani kujulikana, kuwa Baba wa mbinguni mwenye kujali, mwenye kuandaa na mwenye upendo. Kwa wote wanaoamini, haitoshi kumjua Mungu tu kama Mwenyezi, Muumba, Bwana wa wote. Pia anataka tumjue kuwa Baba yetu wa mbinguni.

“Kwa hiyo msisumbukie ya kesho, kwa maana kesho itajisumbua yenyewe. Yatosha kwa siku taabu yake yenyewe” (Mathayo 6:34). Kwa maneno haya ya wazi, Yesu anatuamuru, “Msiwe na mawazo, wasiwasi hata mmoja, ni nini kinaweza kutokea au kisichoweza kutokea kesho. Huwezi kusaidia chochote kwa kuhangaika. Unapohuzunika, unafanya tu kama watu wa mataifa.”

Tunapaswa kuendelea kumpenda Yesu. Tunapaswa kusonga mbele, tukimtwika yeye fadhaa zetu zote, tutulie katika uaminifu wake. Baba yetu wa mbinguni atahakikisha kwamba tunapewa vitu vyote muhimu maishani.

Nashangaa kama malaika wanatatanishwa na wasiwasi na mahangaiko yote ya wale wanaodai kumwamini Bwana. Kwa viumbe hao wa mbinguni, ni lazima ionekane kuwa ni matusi kwa Mungu kwamba tunahangaika kana kwamba hatuna Baba anayejali mbinguni. Ni maswali gani ya kutatanisha ambayo malaika wanapaswa kujiuliza wenyewe kwa wenyewe kama vile “Je, hawajui kwamba Baba anatutuma kuwasimamia wakati wa hatari? Je, wanawezaje kufadhaika na kuwa na wasiwasi wakati wanajua Mungu ana uwezo wote, mali yote, na anaweza kukidhi mahitaji ya viumbe vyote? Wanawezaje kumshtaki Baba yao wa mbinguni kwa kupuuza kana kwamba yeye si mwaminifu kwa Neno lake?”

Ndege huimba, wakati tunalalamika na kuzungumza juu ya hofu na wasiwasi. Mayungiyungi ya kondeni husimama kwa urefu katika utukufu wao, huku tukinyata na kuinama mbele ya upepo mdogo zaidi wa shida. Hakika una Baba wa mbinguni. Mwamini!