KUTEMBEA KATIKA UTUKUFU

David Wilkerson (1931-2011)

Jambo moja linaloweza kutufanya tuendelee katika nyakati ngumu zinazokuja ni kuelewa utukufu wa Mungu. Sasa, hii inaweza kuonekana kama dhana ya hali ya juu iliyoachwa kwa wanatheolojia, lakini nina hakika somo la utukufu wa Mungu lina thamani halisi kwa kila mwamini wa kweli. Kwa kuifahamu, tunafungua mlango wa maisha ya ushindi.

Utukufu wa Mungu ni ufunuo wa asili na nafsi ya Bwana wetu. Unaweza kukumbuka kutoka katika Agano la Kale kwamba Musa alipata mwonekano halisi wa utukufu wa Mungu. Kabla ya hapo, Bwana alikuwa amemtuma Musa bila maelezo yoyote juu yake mwenyewe isipokuwa maneno, "MIMI NDIMI." Musa alitaka kujua jambo fulani zaidi kuhusu Mungu, kwa hiyo akamsihi, “Bwana, nionyeshe utukufu wako.”

Mungu alijibu kwa kumchukua Musa kando na kumweka kwenye ufa wa mwamba. Maandiko yanasema kwamba alijifunua kwa Musa katika utukufu wake wote (ona Kutoka 34:6-7).

Ninaamini kifungu hiki ni muhimu kwa ufahamu wetu wa Bwana wetu ni nani. Ufunuo wa utukufu wa Mungu una matokeo yenye nguvu kwa wale wanaoupokea na kuomba kwa ajili ya kuuelewa. Hadi wakati huu, Musa alikuwa amemwona Bwana kama Mungu wa sheria na ghadhabu. Akatetemeka kwa hofu mbele za Bwana, akamwomba, akamlilia, na kumsihi kwa niaba ya Israeli. Huu ulikuwa ndio msingi wa uhusiano wake wa ana kwa ana na Bwana.

Alipouona utukufu wa Mungu mara ya kwanza, Musa alichochewa kuabudu. “Musa akafanya haraka, akainamisha kichwa chake hata nchi, akasujudu” (Kutoka 34:8). Je, unaona ukweli wa ajabu unaotuonyesha hapa? Ibada ya kweli hutoka katika mioyo iliyoshindwa na maono ya Mungu. Inategemea ufunuo ambao Mungu hutupatia yeye mwenyewe, wema wake, rehema yake, utayari wake wa kusamehe. Ikiwa tutamsifu Mungu katika roho na kweli, ibada yetu lazima itegemezwe juu ya ukweli huu wa ajabu kumhusu.

Mara tunapopokea ufunuo wa utukufu wa Mungu, ibada yetu haiwezi kujizuia kubadilika. Kwa nini? Kuona utukufu wake kunabadilisha jinsi tunavyoishi! Inaathiri sura na tabia zetu, na kutubadilisha kutoka “utukufu hadi utukufu,” na kutufanya tufanane naye zaidi. Kila ufunuo mpya wa upendo wake na rehema huleta mabadiliko yasiyo ya kawaida.